MWANAFUNZI WA KIDATO CHA PILI ALIYEONESHA UWEZA WAKE NA UZALENDO KATIKA MASOMO YAKE.
Malipo ya Sh15,000 anayodaiwa shule, yanaweza kuonekana kuwa ndio chanzo
 cha kupoteza mwelekeo kwa binti wa miaka 14, Rachel Sunguya.
Lakini hilo laweza kuwa ni jibu la haraka haraka; binti huyo amekimbia 
mila potofu za unyanyasaji na ukatili dhidi ya watoto wa kike.
Kwa sasa, Rachel, ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha pili katika Shule 
ya Sekondari ya Benjamin Mkapa iliyo wilayani Simanjiro, amekimbia 
nyumbani kwao kukwepa ndoa ya lazima. Amehifadhiwa Arusha na msamaria 
mwema, lakini hana uhakika wa kuendelea na masomo licha ya kuwa na nia 
ya dhati ya kusoma.
“Kwa zaidi ya wiki tatu nilikuwa nyumbani. Nilirudishwa kutokana na 
kudaiwa mchango huo na nilipomwambia baba alipe, aligoma na baadaye 
nilimsikia akipanga niolewe,” anasema wakati akisimulia mkasa wake.
Rachael anasema baba yake alimwambia kuwa ni lazima aolewe kwani hana fedha za kumlipia ada mtoto wa kike.
“Baada ya kupata taarifa hii na kubaini kuna mipango ilikuwa inafanywa 
niolewe, niliamua kukimbilia hapa Arusha Mjini ili kupata msaada wa 
kuendelee na masomo,” anasema.
Anasema katika familia yao, wapo watoto 15 na baba yake ambaye ni 
mfugaji, mwenyeji wa Kata ya Komolo, Wilaya ya Simanjiro ana wake wanne.
“Mama yangu aliondoka nyumbani miaka mitano iliyopita na sijui alipo,” anasema.
Anasema kwa mama yake, yeye alizaliwa peke yake na hana mdogo wake, ila 
kuna watoto wengine wa kiume katika familia hiyo, wanaendelea na masomo.
“Yupo Baraka ambaye anasoma kidato cha tatu na amekuwa akilipiwa ada,” anasema.
Anasema kwa sasa ataendelea kukaa Arusha, hadi hapo atakapopata msamaria
 mwema ili kumsomesha kwa kuwa hataki tena kurejea nyumbani.
Apeleka malalamiko polisi
Jitihada za mtoto huyo, kuomba kusaidiwa na Dawati la Jinsia katika 
Kituo Kikuu cha Polisi, Arusha zilikwama, baada ya kutoa maelezo na 
kutakiwa kurejea nyumbani wakati suala lake likifuatiliwa.
“Nimeenda polisi, nimetoa maelezo, lakini, nimeambiwa nirudi nyumbani, 
watafuatilia. Sasa, nitarudi vipi wakati hawataki nisome wanataka 
niolewe mimi nimeamua kubaki mjini,” anasema.
Mtoto huyo alisema kwamba anakumbuka akiwa darasa la tatu alichukuliwa 
na wenzake na kwenda kufanyiwa tohara kwa nguvu, lakini licha ya kwenda 
kulalamika polisi hakuna hatua zilizochukuliwa.
“Nakumbuka kipindi kile tulilalamika polisi na wakaja nyumbani, lakini 
hakuna hatua zilizochukuliwa badala yake mimi nilionekana adui katika 
familia na hata kutengwa,” anasema.
Mwalimu mkuu azungumza
Mwalimu mkuu wa Shule ya Sekondari ya Benjamin Mkapa, Emanuel Karo anakiri kumfahamu mwanafunzi huyo anayesoma kidato cha pili.
Hata hivyo, anasema kwa zaidi ya mwezi mmoja sasa hajaonekana shuleni na hajulikani alipo.
Anasema mwanafunzi huyo anatakiwa kujiandaa na mtihani wa kidato cha pili mwaka huu, ambao utafanyika mwezi ujao.
“Nashukuru kwa kunipa taarifa hii kuwa huyu mtoto yupo huko Arusha. Sisi
 huku hatujui wala wazazi wake hawajui alipo na hawajafika hapa kutoa 
taarifa yoyote,” anasema.
Mwalimu huyo, anatoa wito kusaidia mtoto huyo, wa kike ili aweze kufanya
 mtihani wa kidato cha pili wakati taratibu nyingine zikifuatwa.
“Tunaomba aletwe kufanya mtihani wa kidato cha pili kwani hatuna taarifa
 zake na ni kweli amekuwa na matatizo ada na michango mbalimbali 
kutowasilishwa,” anasema.
Mwalimu anakiri kuwa wazazi wa mtoto huyo wamekuwa hawatoi ushirikiano 
kwa uongozi wa shule kwa kulipa ada na michango, jambo ambalo linaathiri
 maendeleo yake.
Mlezi aliyemhifadhi azungumza
Haruna Idd, msamaria mwema, ambaye alimwokota mtoto huyo akiwa eneo la 
Kituo cha Mabasi Arusha anasema: “Nilikuwa katika kazi zangu nikamuona 
huyu binti amezungukwa na vijana. Baada ya kumhoji ndipo alinipa 
historia yake,” anasema.
Anasema mtoto huyo, alieleza kuwa ametoroka nyumbani, kwa kuwa anataka 
kuolewa kwa nguvu na anataka msaada wa kusoma na hana ndugu yoyote hapa 
Arusha Mjini.
“Baada ya maelezo hayo niliamua kumchukua ili kumuepusha na vijana ambao walikuwa tayari wameanza kumzengea,” anasema.
Hata hivyo, anasema yeye hana uwezo wa kumsomesha kwa kuwa hana fedha na kwa zaidi ya mwezi mmoja, amekuwa naye nyumbani kwake.
“Tunaomba watu wenye uwezo wajitokeze kumsaidia kwa kuwa baada ya 
kumpeleka polisi na alipotakiwa kurejea nyumbani kwao, aligoma,” 
anasema.

 
 
 
Comments
Post a Comment