MASAA 72 BAADA YA PINDA KUTANGAZA NIA YA KUWANIA URAISI W JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA MAKADA WA CCM ROHO JUU.
Mzee wa busara Mh.MIZENGO PETER PINDA .baada ya kutangaza nia ya kugombea uraisi mwaka 2015.
SIKU
 moja baada ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kutangaza nia ya kujitosa 
kuwani urais katika Uchaguzi Mkuu 2015, baadhi ya wanachama wa CCM na 
wasomi wamekuwa na maoni tofauti.
Hali
 hiyo imekuwa tofauti ambapo Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Philip 
Mangula, alishindwa kueleza kwa undani kauli hiyo ya Pinda huku akisema 
hawezi kuzungumza jambo lolote kwa sasa hadi pale atakapomaliza vikao 
vya chama.
Akizungumza na MTANZANIA jana kwa njia ya simu, Mangula alisema: “Kwa sasa sina la  kusema kuhusu suala hili kwani nipo kwenye vikao, ninaomba nitafute baadaye ndugu yangu,” alisema kwa kifupi.
Mangula
 ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati Ndogo ya Nidhamu na Maadili ya CCM, hivi
 karibuni alitangaza mikakati ya chama katika kuwadhibiti wagombea 
wanaotangaza nia za kuwania nafasi za uongozi ikiwemo urais kabla ya 
wakati kwa kuwafungulia majalada kila mkoa kwa ajili ya kufuatilia 
mienendo ya wagombea hao.
Pamoja na kuomba atafutwe baada ya saa mbili, MTANZANIA lilifanya hivyo na simu yake alikuwa amezima hadi tunakwenda mitamboni.
Pamoja
 na hali hiyo, MTANZANIA pia lilimtafuta Katibu wa NEC, Itikadi na 
Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye, ambaye simu yake 
iliita bila kupokelewa na hata alipotumiwa ujumbe mfupi wa simu 
hakujibu.
Akizungumzia
 uamuzi huo wa Pinda, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Ali Keissy Mohamed 
(CCM), alimmwagia sifa Waziri Mkuu Pinda kwa kusema ni kiongozi mwenye 
uwezo na asiye na kashfa ya aina yoyote ndani na nje ya Serikali.
Alisema
 kuwa kutokana na sifa yake hiyo, ni wazi kiongozi huyo wa Serikali 
hakukurupuka kuitaka nafasi hiyo ya uongozi wa juu ya nchi.
Hata
 hivyo, alipoulizwa kuhusu mkakati wake wa kugawa fedha kwa wajumbe wa 
CCM waliokwenda katika kikao chake, Keissy alisema hakubaliani na 
taarifa hizo kwa Waziri Pinda kutoa kiasi cha Sh 50,000 kwa wajumbe wa 
Mkutano Mkuu wa CCM Taifa waliofikia 50 toka katika mikoa sita ya Kanda 
ya Ziwa.
Wajumbe
 wa mikoa hiyo wanaodaiwa kupewa kila mmoja Sh 50,000 kwa ajili ya fedha
 za nauli ni wa kutoka kwenye mikoa ya Simiyu, Mwanza, Geita, Mara, 
Shinyanga na Kagera ambao walikutana na Waziri Mkuu Pinda Ikulu ndogo ya
 jijini Mwanza.
“Hiyo
 si kweli kwani Waziri Pinda namjua hana fedha hiyo ya kuwagawia wajumbe
 wote hao, lakini kama kweli katoa atakuwa amefanya makosa, ila kwa 
kutangaza nia bado si kosa kwani kosa ni kufanya kampeni,” alisema.
Kwa
 upande wake, Mhadhiri wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Dar es Salaam Kitivo 
cha Elimu (DUCE), Profesa Kitila Mkumbo, alisema kwa sasa hawezi 
kuzungumzia jambo liolote kuhusu kufaa au kutofaa kwa Waziri Pinda 
kuwania urais mwaka 2015.
“Imekuwa
 kawaida kwa mawaziri wakuu wa nchi hii kila mmoja pindi anapomaliza 
muda wake kutangaza nia ya kuwania urais, hivyo kwa suala la Pinda kama 
anafaa au hafai sina ‘comment’ kwa hilo,” alisema Profesa Kitila.
Inadaiwa
 Pinda pamoja na kugawa fedha hizo kwa kumtumia mmoja wa watu wake wa 
karibu, kugawa nauli ya Sh 50,000 kwa kila mjumbe, ambapo wajumbe hao 
waligomea posho hiyo kwa kueleza kuwa ni ndogo.
Pia
 Waziri Mkuu Pinda anatuhumiwa kutumia harambee ya Taasisi ya Benjamin 
Mkapa kujiimarisha kisiasa, kwani tayari CCM imepiga marufuku kwa 
viongozi wake na makada wake kuendesha harambee zozote zile zenye 
malengo ya kujiimarisha.
Waziri
 Mkuu Pinda aliwaeleza wajumbe hao kuwa baada ya kujitathimini na 
kupokea ushauri toka kwa baadhi ya maaskofu hapa nchini, kwa nia ya 
dhati kabisa ameamua kugombea urais kupitia CCM na kuwataka wajumbe hao 
wa mkutano mkuu kumuunga mkono.
Waziri
 Mkuu Pinda anadaiwa kuwaeleza wajumbe hao kuwa awali hakuwa na nia ya 
kugombea nafasi hiyo kutokana na mazingira ya nafasi yenyewe yalivyo, na
 kueleza kuwa hivi sasa ana ujasiri wa kugombea nafasi hiyo.
Waziri
 Mkuu Pinda anadaiwa kueleza wajumbe hao kuwa ana siri nzito moyoni kwa 
kuwa yeye ni Mjumbe wa Kamati ya Maadili, Kamati Kuu (CCM) na NEC na 
kutamba kuwa ana uhakika jina lake ni miongoni mwa majina matano ambayo 
yatapendekezwa na CC.
Alisema
 kuwa kutokana na mazingira hayo, ndio maana ameamua kukutana na wajumbe
 wa Mkutano Mkuu wa CCM Taifa kwa ajili ya kuwaeleza nia yake ya 
kugombea nafasi hiyo ili waweze kumuunga mkono.
Kauli tata za Pinda
Januari
 25, mwaka 2012, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alitamka hadharani kwamba 
hana nia wala hataki kuwania urais mwaka 2015 Rais Jakaya Kikwete 
atakapomaliza muda wake, kwa kuwa kazi hiyo ni mzigo.
Badala
 yake alisisitiza kuwa hatajisumbua kuingia katika kinyang’anyiro hicho 
kwani amejipanga vyema kuanza maisha mapya ya kufuga nyuki baada ya 
kustaafu.
Kauli
 hiyo ya Pinda aliitoa mbele ya wahariri na waandishi wa habari kuhusu 
mwelekeo wa nchi na masuala muhimu ya kitaifa yaliyojitokeza siku za 
hivi karibuni.
Alisema mwaka 2015 atakuwa mtu mzima sana na haamini kuwa kwa umri huo ataweza kuyamudu majukumu ya nafasi ya urais.
“Niliposema
 sitawania urais nilimaanisha hivyo na naomba watu wanielewe, urais si 
kazi ya kukimbilia kama kweli unataka kuwatumikia watu, kwa wale 
wanaotaka kwenda kuchuma sawa ni pazuri, lakini mimi naona ni mzigo, 
kuna wakati namwonea huruma Rais Kikwete maana kila kitu kigumu 
anaangushiwa yeye,” alisema.
“Mwaka
 2015 nitakuwa na umri wa miaka 67, ina maana nikipata urais baada ya 
miaka mitano nitakuwa na 72, yanini nifike kote huko kwanini wakati 
nimeshalitumikia taifa langu muda mrefu sana, nimefanyakazi ya taaluma 
yangu ya sheria miaka mitatu tu nikaenda Ikulu ambako nimefanyakazi hadi
 leo hii, nimefanyakazi na Mwalimu Nyerere, nimefanyakazi na Mzee 
Mwinyi, Mzee Mkapa na hii awamu ya nne, kama watu hawajaridhika na 
mchango nilioutoa kwa nchi yangu inamaana hata nikiwa nani 
hawataridhika. Urais siutaki na wala siwazii wanaotaka waendelee tu,” alisema.
“Kuna
 wakati nikisema sitaki urais watu wananiambia acha kusema hivyo wewe, 
acha kabisa mzee usiseme hivyo, lakini mimi huwa nawaambia watu hawa 
kuwa huu ni uamuzi wangu na nataka Watanzania waelewe hivyo, anayetaka 
haya! Ila mimi sitakuwemo,” alisema.
Alisema
 anataka baada ya kustaafu ajikite zaidi katika ufugaji wa nyuki kwani 
amebaini kuwa biashara hiyo ina faida sana lakini Watanzania wengi bado 
hawajabaini fursa hiyo.
 
chanzo: Mtanzania
chanzo: Mtanzania


 
 
 
Comments
Post a Comment